06/08/2026
TFNC YATOA WITO KWA WAJASIRIAMALI NANENANE: NJOONI MJIFUNZE UANDAAJI SAHIHI WA UNGA MCHANGANYIKO
Dodoma, na Mwandishi Wetu.
Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC) imetoa wito kwa wajasiriamali na wazalishaji wa unga mchanganyiko wa vyakula vya watoto kutembelea banda lao katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane ya yanayoendelea kufanyika jijini Dodoma katika Viwanja vya Dkt. John Samweli Malecela Nzuguni, ili kujifunza dondoo muhimu za namna ya kuandaa unga huo kwa usahihi.
Wito huo umetolewa Afisa Lishe Mtafiti kutoka TFNC, Stephano Ngunzwa, wakati akizungumza kuhusu umuhimu wa lishe bora kwa makundi maalumu, hususan watoto wadogo wenye umri wa kati ya miezi 6 hadi 23.
“Tunawakaribisha wajasiriamali na wazalishaji wote wanaofanya biashara hii au wanaonuia kuanza, waje kwenye banda letu. Lengo letu ni kuwapa miongozo na dondoo sahihi za namna ya kuandaa unga mchanganyiko (composite flour) unaokidhi vigezo vya afya na ukuaji bora wa mtoto,” alisema Ngunzwa.
Aida Nguzwa amesema Wajasiriamali watakaotembelea banda la TFNC watanufaika na mafunzo ya vitendo yanayohusu:
* Uwiano Sahihi wa Nafaka: Namna ya kuchanganya nafaka, mikunde, na mbegu za mafuta bila kuharibu mfumo wa usagaji chakula wa mtoto.
* Usafi na Usalama wa Chakula: Mbinu za kuzuia sumukuvu (aflatoxins) wakati wa kukausha na kusaga mazao.
* Uongezaji wa Thamani: Jinsi ya kuzalisha bidhaa zinazokubalika sokoni kulingana na miongozo ya ubora wa chakula nchini.
Ushiriki wa TFNC kwenye maonesho ya mwaka huu unaenda sambamba na kaulimbiu ya Nanenane 2026 inayosisitiza utambuzi wa soko na kuongeza tija kuelekea Dira ya Maendeleo ya 2050. Kupitia elimu hii, taasisi inalenga kutokomeza udumavu na utapiamlo kwa watoto, huku ikisaidia wajasiriamali wa ndani kuzalisha bidhaa salama na zenye ushindani wa kibiashara.
Maonesho ya Nanenane yanatarajiwa kilele chake tarehe 8 Agosti 2026, hivyo wananchi na wadau wote wa lishe wanahimizwa kufika viwanjani hapo mapema kujipatia maarifa.